Timu ya
soka ya Taifa ya Tanzania, Taifa Stars imefungwa mabao 4-2 dhidi ya Ivory Coast
na kuzima harakati zake za kufuzu kucheza fainali za Kombe la Dunia 2014 huko
Brazil.
Watanzania
wengi na wadau wa michezo walidhani Taifa Stars ingeweza kusonga mbele katika
harakati hizo za kufuzu kucheza Kombe la Dunia 2014, lakini sasa ukweli
umejidhihirisha.
Sasa
wengi wamekubaliana na uhalisia wa mambo kwamba, inahitaji muda kidogo kuona
Taifa Stars ikisonga mbele katika kuelekea kufuzu Kombe la Dunia na siyo rahisi
kama ilivyodhaniwa hapo kabla.
Ni mambo
mengi yaliyotokea katika mchezo dhidi ya Ivory Coast ambayo yaliigharimu Taifa
Stars licha ya uwanja kujaa idadi kubwa ya mashabiki waliokuwa wakiishangilia
timu yao bila kuchoka.
Jambo la
msingi ni kwamba, Taifa Stars ikiwa katika harakati za kuhakikisha inafuzu
Kombe la Dunia wengi tulisahau kwamba, kwa ‘reality’ ilikuwa ngumu kwa Taifa
Stars kufuzu fainali hizo japokuwa kwa mapenzi tulidhani timu hii ingeweza
kufuzu kwa kuanza na vipigo kwa timu za Morocco na Ivory Coast.
Tukitazama
mchezo kati ya Taifa Stars na Ivory Coast kuna baadhi ya mambo yalionekana
kwamba bado tuna safari ndefu ya kufuzu Kombe la Dunia kama kweli tuna nia ya
kufanya hivyo.
Mambo
mengi mno yalijitokeza katika mchezo kati ya Taifa Stars dhidi ya Ivory Coast
na haya ni machache kati ya mengi yake;
Safu ya
Ulinzi Ilipaparika; Ilikuwa kama kila mchezaji ameahidiwa kiasi
kikubwa cha fedha, kwani mara nyingi wachezaji wa Taifa Stars hawakucheza
katika nafasi zao na hilo liligharimu timu na kujikuta wakilala mabao 4-2.
Erasto
Nyoni ndiye beki anayeweza kuondoka na lawama nyingi lakini halikuwa kosa lake
wakati mwingine kwani alilazimika kwenda katikati kusahihisha makosa ya mabeki
wa kati na kuisahau nafasi yake.
Ilionekana
wazi kwamba yalikuwepo mawasiliano hafifu juu ya kutengeneza mtego wa kuotea
yaani ‘offside trick’ na matokeo yake Ivory Coast walitumia vyema mwanya huo na
kujipatia mabao manne.
Baada ya
kuonekana ‘njia’ tangu dakika za mwanzo, beki Erasto Nyoni inaonekana hakupata
ushauri wa kutosha kuhusu kutulia na kucheza soka kwani hata makelele ya
mashabiki yalimfanya aonekane mtu asiyefaa kikosini. Lakini alikuwepo benchi anayeweza
kumudu nafasi yake moja kwa moja?
Nguvu
hafifu; Wachezaji wengi wa Taifa Stars walionekana kutokuwa na nguvu ya
kupambana na wenzao wa Ivory Coast kutokana na hali halisi ya miili yao.
Sure Boy
mfupi na mwenye mwili mdogo alionekana kama mchezaji wa kawaida mbele ya Yaya
Toure mwenye mwili mkubwa na nguvu, na mara nyingi Toure aliiwahi mipira ambayo
ingeweza kuwahiwa na Sure Boy.
Domayo
naye hakuweza kufua dafu mbele ya Traore Lucina na Jean Jacques ambao wote ni
watu wa miraba minne.
Kikosi cha Ivory Coast
0 Comment to "TAIFA STARS YAFUNGWA NA IVORY COAST 4 - 2"
Post a Comment