Waziri
Mkuu wa Uingereza David Cameron amesema kuwa Somalia "imepiga hatua
kubwa" katika kumaliza fujo na machafuko yaliodumu kwa zaidi ya miongo
miwili.
Bwana Cameron ni
mwenyeji wa mkutano wa kutafuta amani ya kudumu nchini Somalia.
Mkutano huo unalengo la
kumsaidia Rais Hassan Sheikh Mohamud aweze kuijenga tena upya Somalia.
Somalia inahesabiwa kuwa
miongoni mwa mataifa yalioanguka na ambayo imekuwa ikihangaishwa na magaidi wa
Al shabaab, uharamia na ukame ulioitikisa mwaka kati ya 2010 hadi 2012.
Rais Mohamud wa Somalia
amesema serikali yake itafaulu kuidhibiti nchi nzima na kukabiliana na utovu wa
usalama ifikapo mwaka 2015.
Mkutano huo utajikita
zaidi katika masuala ya kujenga upya vikosi vya ulinzi na kukabiliana na
ubakaji ambalo ni suala linalooonekana kama mwiko.
Takriban watu saba
waliuawa katika mlipuko wa bomu kwenye gari uliotokea katika mji mkuu Mogadishu
siku ya Jumapili. Kundi la Al - Shabab ambalo lina mafungamano na Al - Qaeda
linadai kuhusika na shambulio hilo.
Mkutano huo ambao
utakua chini ya uenyekiti wa Bw. Cameron na rais wa Somalia Hassan Sheikh
Mahamoud unafuatia mkutano kama huo uliofanyika London na jijini Istanbul
nchini uturuki mwaka jana, huku wasiwasi ukiongezeka katika jumuiya ya
kimataifa kwamba Somalia imegeuka hifadhi ya wanamgambo wenye mahusiano na al
Qaeda.
"Ninamatumaini
kwamba, wote tunaweza kuafikiana kuhusu mpango wa usalama wa muda mrefu, ambao
utamaliza vitisho vya Al Shabab moja kwa moja," alisema Bw. Cameron.
"Pia ninamatumaini
tutaboresha uwazi na uwajibikaji ili watu wafahamu wapi rasilimali zinakwenda.
Pia tunahitaji kuendelea na mchakato wa kulijenga taifa la Somalia, ikiwemo
mikoa yote ya Somalia na nchi jirani hali kadhalika."
Mchambuzi wa masuala ya
Somalia wa BBC, Mary Harper anasema, kumekuwa na mabadiliko ya ghafla nchini
humo katika kipindi cha mwaka mmoja uliopita.
Kuna serikali mpya, ya
kwanza katika kipindi cha zaidi ya miongo miwili kutambuliwa na Marekani,
Shirika la Fedha la Kimataifa (IMF) na wadau wengine muhimu, anasema.
0 Comment to "DAVID CAMERON: "SOMALIA IMEPIGA HATUA""
Post a Comment