Rais Xi Jinping, rais wa Uchina, ametia saini
mikataba kadha na Rais Jakaya Kikwete wa Tanzania mjini Dar-es-salaam.
Rais Xi aliingia
Dar-es-salaam akitokea Moscow ambako ndiko alikoanza safari yake ya kwanza
katika nchi za nje tangu kutawazwa rasmi kuwa rais hivi karibuni.
Hapo awali
alipokelewa kwa ngoma na mizinga.
Rais Xi alitia
saini mikataba 17 ya uchumi na utamaduni, mojawapo ni kuhusu ujenzi wa bandari
mpya Bagamoyo pamoja na reli itayoungana na reli nyengine za Tanzania.
Akizungumza
ikulu mjini Dar-es-salaam, kiongozi wa Uchina alisema ziara yake ni ishara ya
uhusiano mwema kati ya nchi mbili hizo ambao umeendelea tangu ulipoanza wakati
wa Rais Julius Nyerere na Mao Zedong.
Safari yake
barani Afrika inaonesha umuhimu wa Afrika kwa Uchina, kuwa ni chanzo cha madini
na nishati na piya soko kwa bidhaa za Uchina.
Rais wa Uchina
anatarajiwa kutoa hotuba muhimu leo Jumatatu kuhusu uhusiano baina ya Uchina na
Afrika.
Uchina ni ya
pili katika uwekezaji nchini Tanzania, baada ya Uingereza.
Bwana Xi piya
anapanga kuzuru Afrika Kusini ambako viongozi wa mataifa ya uchumi
unaochipukia, BRICS, watakutana Jumaane mjini Durban.
Baada ya hapo
anapanga kuzuru Congo.
0 Comment to "RAIS JINPING AKUTANA NA KIKWETE DAR-ES-SALAAM"
Post a Comment