Sunday, April 21, 2013

LUIS SUAREZ AMEOMBA RADHI KWA KUMNG'ATA BRANISLAV IVANOVIC

Ivanovic akimuonyesha mwamuzi alivyong`atwa

Branislav Ivanovic na Luis Suarez

Mshambuliaji wa Liverpool Luis Suarez ameomba radhi kutokana na kitendo chake cha kumng'ata mkononi beki wa Chelsea Branislav Ivanovic wakati timu hizo mbili zilipocheza jumapili jioni kwenye mchezo wa ligi kuu soka nchini Uingereza.

Suarez,amesema binafsi anasikitishwa na kitendo alichokifanya na amempigia simu Ivanovic na kumuomba radhi yeye mwenyewe kwani anajutia kitendo alichomfanyia,na kushuruku kwa kuwa Ivanovic amemsamehe.

Kitendo hicho kilitokea katika kipindi cha pili cha mechi baina ya Liverpool na Chelsea,Mechi iliyoishia kwa sare ya 2-2 huku Suarez akifunga bao la dakika za mwisho la kuisawazishia Liverpool. Ivanovic alimuonyesha mwamuzi Kevin Friend sehemu aliyong'atwa na Suarez lakini mwamuzi alionekana kutotilia maanani kwa kuwa hakukiona kitendo hicho.

Wachambuzi wa masuala ya kandanda nchini Uingereza wamekitaja kitendo hicho cha Suarez kama tukio lisilokubalika katika mchezo wa soka,huku wakisema huenda akakabiliwa na adhabu kali kutoka chama cha soka nchini Uingereza FA.

Kocha wa Liverpool, Brendan Rodgers amesema ameangalia video ya tukio hilo mara baada ya mchezo na amesikitishwa na kitendo hicho na kumueleza Suarez kuwa kitendo hicho hakikubaliki michezoni,huku akisisitza kuwa hakuna mchezaji ambaye ni mkubwa zaidi ya klabu hiyo. Naye Mkurugenzi wa klabu hiyo ya Liverpool Ian Ayre amesema kitendo alichokifanya Suarez hakistahili kufanywa na mchezaji wa klabu hiyo.

Liverpool imesema itatoa adhabu stahili kwa kitendo hicho wakati wakisubiri adhabu yoyote kutoka chama cha soka cha Uingereza FA.

Suarez sio wa kwanza kufanya kitendo cha kumng'ata mchezaji uwanjani kwenye ligi kuu ya Uingereza,kwani mwaka 2006, mshambuliaji wa Tottenham Hotspur Jermain Defoe alimng'ata kiungo wa West Ham wa wakati huo Javier Mascherano katika mchezo wa ligi kuu kwenye uwanja wa White Hart Lane.

Defoe alifanya kitendo hicho baada ya kuchukizwa na rafu aliyochezewa na Mascherano ambapo mwamuzi Steve Bennett aliwazawadia kadi za manjano wote wawili na baadaye chama cha soka cha Uingereza FA kilisema hakitoa adhabu yoyote kwa kuwa mwamuzi alikiona kitendo hicho na kuwaadhibu uwanjani.





Share this

0 Comment to "LUIS SUAREZ AMEOMBA RADHI KWA KUMNG'ATA BRANISLAV IVANOVIC"

Post a Comment