Ivanovic akimuonyesha mwamuzi alivyong`atwa
Branislav Ivanovic na
Luis Suarez
Mshambuliaji wa
Liverpool Luis Suarez ameomba radhi kutokana na kitendo chake cha kumng'ata
mkononi beki wa Chelsea Branislav Ivanovic wakati timu hizo mbili zilipocheza
jumapili jioni kwenye mchezo wa ligi kuu soka nchini Uingereza.
Suarez,amesema binafsi
anasikitishwa na kitendo alichokifanya na amempigia simu Ivanovic na kumuomba
radhi yeye mwenyewe kwani anajutia kitendo alichomfanyia,na kushuruku kwa kuwa
Ivanovic amemsamehe.
Kitendo hicho kilitokea
katika kipindi cha pili cha mechi baina ya Liverpool na Chelsea,Mechi
iliyoishia kwa sare ya 2-2 huku Suarez akifunga bao la dakika za mwisho la
kuisawazishia Liverpool. Ivanovic alimuonyesha mwamuzi Kevin Friend sehemu
aliyong'atwa na Suarez lakini mwamuzi alionekana kutotilia maanani kwa kuwa
hakukiona kitendo hicho.
Wachambuzi wa masuala
ya kandanda nchini Uingereza wamekitaja kitendo hicho cha Suarez kama tukio
lisilokubalika katika mchezo wa soka,huku wakisema huenda akakabiliwa na adhabu
kali kutoka chama cha soka nchini Uingereza FA.
Kocha wa Liverpool,
Brendan Rodgers amesema ameangalia video ya tukio hilo mara baada ya mchezo na
amesikitishwa na kitendo hicho na kumueleza Suarez kuwa kitendo hicho
hakikubaliki michezoni,huku akisisitza kuwa hakuna mchezaji ambaye ni mkubwa
zaidi ya klabu hiyo. Naye Mkurugenzi wa klabu hiyo ya Liverpool Ian Ayre
amesema kitendo alichokifanya Suarez hakistahili kufanywa na mchezaji wa klabu
hiyo.
Liverpool imesema
itatoa adhabu stahili kwa kitendo hicho wakati wakisubiri adhabu yoyote kutoka
chama cha soka cha Uingereza FA.
Suarez sio wa kwanza
kufanya kitendo cha kumng'ata mchezaji uwanjani kwenye ligi kuu ya
Uingereza,kwani mwaka 2006, mshambuliaji wa Tottenham Hotspur Jermain Defoe
alimng'ata kiungo wa West Ham wa wakati huo Javier Mascherano katika mchezo wa
ligi kuu kwenye uwanja wa White Hart Lane.
Defoe alifanya kitendo
hicho baada ya kuchukizwa na rafu aliyochezewa na Mascherano ambapo mwamuzi
Steve Bennett aliwazawadia kadi za manjano wote wawili na baadaye chama cha
soka cha Uingereza FA kilisema hakitoa adhabu yoyote kwa kuwa mwamuzi alikiona
kitendo hicho na kuwaadhibu uwanjani.
0 Comment to "LUIS SUAREZ AMEOMBA RADHI KWA KUMNG'ATA BRANISLAV IVANOVIC"
Post a Comment